HAIKUWA kazi rahisi kuwashawishi Watanzania kuangalia mechi za Ligi Kuu na kuacha Ligi ya England, au kulazimika kuangalia kwa pamoja.
Ni kazi ngumu iliyofanyika kuwashawishi na kwa sasa Ligi ya Tanzania ni moja kati ya ligi zinazoangaliwa na watu wengi si hapa tu, bali ukanda wote huu wa Afrika Mashariki na Kati hadi Kusini.

Ni watu waliamua kuacha kazi na kufanya kazi, kuna watu waliwashawishi mashabiki kwa kuwekeza kwenye soka, yapo makampuni mengi yameanza kujitokeza kudhamini klabu pamoja na soka lenyewe kwa ujumla kupitia Shirikisho la Soka nchini (TFF).

Wapo watu binafsi ambao nao baada ya kuona soka limeanza kuwa na mvuto kwa mashabiki, wamewekeza kwenye klabu walitoa pesa nyingi, si kwa ajili ya wao kupata faida, bali kuufanya mchezo wa soka kuendelea kuwa kituvio, lakini kuendelea kutengeneza vijana kwa ajili ya timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars.

Wakati TFF, makampuni, na wadau wakilifanya soka la Tanzania kung'ara ndani na nje ya mipaka ya nchi, kumeanza kutokea mambo ya ajabu yanayotaka kurudisha soka la Tanzania kwenye zama za giza. Si wengine ni baadhi ya waamuzi.


Waamuzi ni moja kati ya watu ambao wanafanya soka la nchi liendelee, kuwa na ligi bora au mbovu, pia kutoa mwakilishi bora kwenye mechi za kimataifa, kutoa mwakilishi dhaifu na feki.

Pamoja na kwamba Ligi Kuu ya Tanzania imeanza kwa mvuto, kuwa ngumu kutokana na kila timu kuonekana kujipanga kisawasawa, huku zikichagizwa na pesa zilizowekwa na wadhamini Azam Media, pamoja na NBC, baadhi ya waamuzi wameonekana kuanza kuharibu mapema kabisa.

Hata mzunguko wa kwanza haujafika kumekuwa na matukio mengi ambayo waamuzi wametoa maamuzi yasiyo sahihi na kuzipokonya timu ushindi au sare.